MAHABA NIUE NICHIMBIE SHIMO UNIFUKIE WEMA, DIAMOND WAZINDUA GARI KWA KULANA DENDA


Mahaba nimalize! Mastaa wapendanao, Wema Isaac Sepetu ‘Madam’ na Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ wamesababisha tukio jipya kama kawaida yao, safari hii wameishtua kadamnasi kwa kuzindua gari jipya kwa mahaba mazito ndani yake, Ijumaa Wikienda lilinyaka mchongo mzima.

Mastaa wapendanao, Wema Isaac Sepetu ‘Madam’ na Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ wakikumbatiana kimahaba.
KAMA MUVI YA MAPENZI
Tukio hilo lililojiri kama muvi ya mapenzi (romantic movie) lilitokea mwishoni mwa wiki iliyopita kwenye Ukumbi wa Golden Jubilee uliopo Posta jijini Dar wakati Diamond alipokuwa akisherehekea siku yake ya kuzaliwa na kujizawadia ndinga aina ya BMW X6 ambalo waliligeuza kuwa uwanja wa malovee wakati walipokwenda kukabidhiwa na menejimenti yake ya Wasafi.
SHEREHE ILIVYOANZA
Awali, waalikwa sambamba na mastaa mbalimbali wakusanyika kwenye ukumbi huo na ilipofika saa 5:00 usiku, Diamond akiwa ameambatana na ubavu wake, Wema sambamba na mama yake mzazi, Sanura Kassim ‘Sandra’, waliingia na sherehe kuanza.
Wema Isaac Sepetu ‘Madam’ na Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ wakila 'romansi'.
TUKIO LA ZAWADI
Baada ya sherehe hiyo kupambwa na matukio mbalimbali zikiwemo bendi za asili na wasanii, ulifika wakati wa zawadi ndipo wageni waalikwa walipoanza kujinadi kupitia kipaza sauti na mwishoni ikawa ni zamu ya menejimenti ya Wasafi ambayo ilitamka kuwa inatoa gari hilo.
CHIEF KIUMBE NDANI
Pedeshee maarufu Bongo ambaye kwa sasa amemrudia Mungu na kuwa mtu wa ibada, Chief Kiumbe hakuwa nyuma katika eneo la zawadi, alifanya kufuru kwa kumrushia Diamond mabunda ya dola za Kimarekani.
Mapaparazi wakidaka mchongo mzima laivu.
BABU TALE SASA!
Baada ya kufuru ya kurushiwa ‘madolari’, funga kazi ya zawadi ilimaliziwa na meneja wa msanii huyo, Bab Tale aliyepanda jukwaani na kutangaza kuwa uongozi na familia ya mwanamuziki huyo wamemnunulia gari jipya aina ya BMW X6 na kumtaka ampeleke lilipoegeshwa amkabidhi.
WATU WASHUKA UKUMBINI
Kwa kuwa ukumbi huo upo ghorofani, waalikwa wote sambamba na ‘birthday boy’, Dangote au Chibu, walishuka kwa kutumia lifti za jengo hilo kwenda kuliona gari hilo lililokuwa limeegeshwa katika ‘parking’ maalum.
Wakitoka kwenye ndinga(BMW) kuendelea na sherehe nzima ya bethidei.
MAMA AKABIDHI
Mbwembwe na mikogo ya kimahaba kati ya Diamond na Wema iliendelea hadi pale mama Diamond, Sandra alipomkabidhi mwanaye huyo funguo za gari hilo, wakazama ndani.
MAHABA MAZITO
Kitendo cha wawili hao kuingia ndani ya gari hilo lenye thamani ya zaidi ya Sh. milioni 90 za Kitanzania na kufunga milango, kilikuwa ni mwanya mzuri kwao kuanza kuoneshana mahaba motomoto ambapo Diamond alimminia mtoto wa kike mabusu ya kumwaga kisha kugandana kama kumbikumbi.
Hili ni gari jipya aina ya BMW X6 ambalo Diamond amezawadiwa katika sherehe ya bethidei yake.
WATUMIA DAKIKA 20
Wapendanao hao walionekana kuzidisha mahaba ambapo walijifungia ndani ya gari hilo kwa zaidi ya dakika 20 na kufanya yao huku watu wapenda ‘ubuyu’ wakiwachungulia kwa dirishani lakini wale waungwana waliamua kutazama pembeni wasione mambo ya chumbani hadharani.
Baada ya kushuka ndani ya gari hilo, wawili hao walikumbatiana tena na kurudi ukumbini ambapo burudani za kula na kunywa ziliendelea.
KUMBUKUMBU MUHIMU
Hivi karibuni ilifanyika bethidei ya Wema ambapo Diamond alimzawadia mpenzi wake huyo gari aina ya Nissan Murano lenye thamani ya Sh. milioni 36 za madafu huku meneja wa wema, Martin Kadinda akimpa BMW ambalo limeibua mjadala juu ya uhalali wa meneja huyo kuwa na uwezo wa kulinunua.

0 comments:

Copyright © 2013. MAPYATZBLOG - All Rights Reserved
Customized by: MAPYATZBLOG | Powered by: http://bongoswagzs.blogspot.com/
Designed by: http://bongoswagzs.blogspot.com//