Miili ya waliofukiwa kifusi mgodini yaopolewa


Hatimaye wachimbaji wote watatu waliokufa kwa kufukiwa na kifusi cha jabali katika mgodi wa dhahabu wa Onesmo Goldmine Mawemeru uliopo katika kijiji cha Nyalugusu Wilayani Geita imeopolewa jana usiku baada ya juhudi za siku nne.

Hatua hiyo imedaiwa ni matokeo ya ushirikiano na mshikamano mkubwa uliooneshwa katika kutekeleza zoezi hilo kati ya Uongozi wa Mgodi huo, wadau na serikali ya wilaya na mkoa zoezi lililokuwa linafanyika usiku na mchana kwa kushirikisha wadau tofauti na hivyo kufanikiwa.
 
Kamanda wa Polisi mkoa wa Geita Kamishna msaidizi mwandamizi wa polisi Joseph Konyo akithibitisha LEO kupatikana kwa miili hiyo alisema kazi hiyo ilihitaji ujasiri na kujituma na ndicho kilichofanyika kuhakikisha miili yote mitatu imeopolewa.
 
Amewataja miili yao walioopolewa kuwa ni Benjamin Yusuph, Robert Edward na Nsulwa Bungila ambao wote walifukiwa katika mgodi huo Januari 11 saa moja usiku na wengine wanne Samson Haroun, Rutu William, Faida Bukombe na Seif Ally waliokolewa siku ya tukio.
 
Akizungumzia hatua hiyo jana Mkurugenzi wa Mgodi huo Malugu Onesimo Gelewa alisema toka usiku tukio la ajali lilipotokea wamekuwa wakifanya kazi usiku na mchana ya kuitafuta miili hiyo chini ya mafundi na wadau wengine na hatimaye kufanikiwa.
 
''Miili yote mitatu imepatikana usiku wa kuamkia leo Januari 15, kwa nyakati tofauti na mwili wa mwisho ambao ni watatu umepatikana alfajiri ya kuamkia jana na tayari imesafarishwa kwa ajili ya maziko makwao.
 
Awali akitoa salaam za rambirambi za serikali kwenye eneo la tukio mkuu wa mkoa wa Geita Fatma Mwasa Juzi aliwaomba wananchi wakiwemo waliofikwa na msiba huo kuwa wavumilivu kutokana na ajali hiyo na kusisitiza watu wote ikiwemo serikali ilikuwa imeguswa na msiba huo na kutaka tahadhari zaidi kuchukuliwa.
 
Peter Fungameza mmoja wa wafanyakazi wa mgodi huo amesema ajali hiyo ilitokea Januari 11 saa moja usiku baada ya kile kinachodaiwa jabali kuporomoka ghafla kwa ndani katika shimo hilo namba 1A na kusababisha ajali hiyo katika mazingira ya kushtukiza.
 
Aliongeza kuwa utendaji kazi katika mgodi huo umekuwa unafanyika kwa kuzingatia ratiba, pamoja na shimo kukaguliwa kila siku kabla ya kuanza kufanya kazi na baada ya kazi kila siku na hata siku ya ajali inatokea ulikuwa umefanywa na wakaguzi wa mgodi huo.

0 comments:

Copyright © 2013. MAPYATZBLOG - All Rights Reserved
Customized by: MAPYATZBLOG | Powered by: http://bongoswagzs.blogspot.com/
Designed by: http://bongoswagzs.blogspot.com//